MZIGO WA MIFUKO 150 YA CHOKAA WAPOKELEWA NA WANACHAMA WA TWENDE PAMOJA AMCOS
Wanachama wa Twende Pamoja AMCOS Limited wamepokea mzigo wa mifuko 150 ya chokaa utakaotumika kuboresha rutuba ya udongo na kuongeza uzalishaji mashambani.
Makabidhiano ya mzigo huo yalifanyika tarehe 11 Februari 2026, ambapo Mwenyekiti wa Bodi, Todos Leonard Msigwa, alipokea mzigo huo kutoka kwa Emmakrata Kyando, Afisa Masoko wa Guavay Company Limited.
Akizungumza wakati wa mapokezi hayo, uongozi wa AMCOS ulieleza kuwa upatikanaji wa chokaa hiyo ni hatua muhimu katika kukabiliana na changamoto ya tindikali kwenye udongo ambayo imekuwa ikiathiri uzalishaji wa mazao kwa baadhi ya wakulima. Matumizi ya chokaa yanatarajiwa kuongeza rutuba ya udongo, kuboresha afya ya mazao na kuongeza mavuno kwa wanachama.
Aidha, AMCOS imeeleza kuwa itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa pembejeo za kilimo ili kuhakikisha wakulima wanapata huduma na pembejeo bora kwa wakati, hatua itakayosaidia kuongeza tija na kipato kwa wanachama wake.









